̽ѡ

Kuchukua hatua kuhusu hali ya hewa: Vijana Waafrika waanzisha biashara zinazotunza mazingira

Get monthly
e-newsletter

Kuchukua hatua kuhusu hali ya hewa: Vijana Waafrika waanzisha biashara zinazotunza mazingira

Franck Kuwonu
Afrika Upya: 
6 August 2019
Bamboo bikes on display.
Bernice Dapaah/Ghana Bamboo Bikes Initiative
Baiskeli za bamboo kwenye onyesho.

Vijana ndio kiungo muhimu katika kuchukua hatua kuhusu hali ya hewa na mazingira. Huo ndio ujumbe uliowasilishwa kwa wajumbe katika Juma la Afrika kuhusu Mazingira, moja kati ya hafla tatu za kieneo za kila mwaka kuhusu hali ya hewa kabla ya Mkutano Mkuu Kuhusu Hali ya hewa wa Katibu wa Umoja wa Mataifa utakaoandaliwa mnamo Septemba mwaka huu.

Juma la Afrika kuhusu Mazingira lilifanyika jijini Accra, Ghana, na liliandaliwa na serikali ya Ghana na Nairobi Framework Partnership, ambao husaidia mataifa yanayoendelea kutayarisha na kutekeleza mipango yao ya kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa, na mashirika yanayoshirikishwa.

Katika kongamano hilo mwezi wa Machi, wanaharakati asilia wa mazingira walionyesha mabango maridadi yaliyosomeka “Taka nunge zavutia, Chukua Hatua Sasa” na “Plastiki au Karatasi= Ukataji miti, Chuku hatua sasa,” miongoni mwa kaulimbiu nyingine.

Wengi wa Waafrika wachanga, ambao walishiriki Kongamano la Juma la Afrika kuhusu Mazingira wamekuwa wakianzisha biashara ndogondogo zinazokabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa, zinazolinda mazingira na kutoa ajira.

Baadhi ya biashara bunifu zilizoonyeshwa katika kongamano hilo ni pamoja na mpango wa baiskeli za mianzi ambao unatumia uwezo wa kiikolojia wa mianzi, kampuni ya kuunda upya bidhaa za plastiki, na mradi unaounda upya tairi zilizotumika na vitambaa, kugeuza taka kuwa viatu na wakati uo huo kukabiliana na uchafuzi wa mazingira.

Baiskeli za mianzi za Ghana ni maarufu ulimwenguni
Bernice Dapaah, founder and CEO, Ghana Bamboo Bikes Initiative.
Bernice Dapaah, founder and CEO, Ghana Bamboo Bikes Initiative.

“Ni vipi tunavyoweza kutumia malighafi yetu asilia kama mianzi kubuni ajira kama biashara jumuishi kielelezo—biashara inayoweza kukabili masuala ya kimazingira, masuala ya kijamii na kiuchumi?” Hilo ndilo swali alilokuwa akiwazia Bernice Dapaah alipoanzisha kwa kushirikiana mradi wa Ghana Bamboo Bikes Initiative (GBBI) unaotengeneza baiskeli kwa kutumia mianzi mnamo mwongo mmoja uliopita.

Mradi huu wa GBBI upo jijini Kumasi, kusini mwa Ghana na unawaajiri wafanyakazi 500, wengi wakiwa wanawake. Mradi unaunda na kuuza baiskeli zilizoundwa kwa mikono kwa kati ya dola 150 na 300 kila moja.

“Tuna baiskeli za aina mbalimbali. Tunazo baiskeli zinazowafaa wanaume na zile zinazowafaa wanawake. Aidha tuna baiskeli za kukwea milima, za mashindano na za maeneo tambarare, pamoja na baiskeli za kubebea zinazotumiwa na wakulima kubebea mizigo,” Bi. Dapaah liambia Africa Renewal.

Mwaka wa 2018, kampuni iliunda takriban baiskeli 1,000 na hii ni baada ya kuongeza uzalishaji taratibu kwa miaka kadhaa. “Tunatumai kufanya mengi mwaka huu kwa kuwa tutapanua karakana yetu na kuwapa vijana zaidi mafundisho kuhusu uzalishaji,” alisema. Katika miaka ijayo, kampuni inanuia kuunda baiskeli za umeme kwa mianzi, baiskeli za ambulensi za umeme kwa mianzi na baiskeli za makanyagio za teksi kwa mianzi, miongoni mwa miundo mingine.

“Kwa sasa, sehemu za baiskeli hizo zilizoundwa kwa mianzi ni kati ya 75% na 80%. Kiwiliwili chake huundwa kwa mianzi, lakini magurudumu na injini ni za kawaida kama katika baiskeli nyinginezo” Bi. Dapaah alifafanua. Kwake yeye, mpango huu wa baiskeli za mianzi unahusu sio biashara tu; bali pia uwezeshwaji wa wanawake.

Kwa jumla, Bi. Dapaah anafurahi kwamba biashara hiyo sio “taashira ya kimazingira tu. Tunakuza mianzi ili kutimiza mahitaji ya biashara yetu. Tunajaribu pia kupunguza kaboni hewani. Hilo ndilo tunalolifanya. Tunatarajia kufanya mengi zaidi siku za usoni.”

Coliba Ventures: kugeuza uchafu wa plastiki kuwa utajiri

“Moja kati ya mambo wasiyoyajua watu wetu ni kwamba plastiki huchukua miaka mingi kabla ya kuoza mchangani. Na athari zake mbaya huonekana baada ya muda mrefu, na wakati huo, uharibifu wake huwa mkubwa kiasi kwamba hauwezi kudhibitiwa—kwa kuwa uharibifu huo huwa wa hali ya juu,” Wisdom Kafui Honu aliambia Africa Renewal.

Bw. Honu, ambaye ni mwanzilishi mwenza wa Coliba Ventures, biashara moja ya taka za plastiki iliyoko Accra, Ghana, alikuwa akiongea kuhusu jinsi alivyoishia kuwa mjasiriamali wa kimazingira. Yote yalianza kutokana na mkasa wakati mmoja wa marafiki wake aliposombwa na maji ya mafuriko. Kilichosababisha tanzia kilikuwa mikondo ya maji iliyozibwa na taka za plastiki.

Wisdom Kafui Honu, co-founder, Coliba Ventures, Ghana.
Wisdom Kafui Honu, co-founder, Coliba Ventures, Ghana.

“Ilikuwa katika mwezi wa Juni mnamo 2015. Rafiki yangu alikuwa akinisubiri na nilikuwa nimechelewa kufika katika eneo la mkutano huo. Mvua ilianza kunyesha na mafuriko yakatokea upesi katika eneo la njia panda alipokuwa amesimama. Maji ya mafuriko yaligeuka na kuwa kijito kiharibifu ambacho kiliharibu mali, kikasomba magari mbali, na kuzamisha wapitanjia,” alisema.

Zaidi ya watu 50 waliuliwa na maji siku hiyo.

“Ilikuwa mvuaa kubwa,” alikumbuka Bw. Honu. “Lakini sehemu za kupitisha maji zilikuwa zimezibwa na taka za plastiki.”

Huku akiwa amehujumiwa na kifo cha rafiki yake, Bw. Honu alisema kuwa alijiuliza, “Badala ya kuomboleza, mbona usifanye kitu kuihusu hali hii? Mbona usisuluhishe tatizo hili sasa, mbona usiunde upya plastiki ambazo huchukua muda mrefu kuoza?”

Hapo ndipo alipoanzisha kwa kushirikiana Coliba Ventures, kampuni anayoielezaa kama “huduma kamili ya kukomboa na kukusanya plastiki.” Pia, inawaelimisha watu waliozoea kurundika pamoja plastiki na taka nyingine namna ya kuzitenga.

“Huu umekuwa mmoja kati ya mipango migumu zaidi kwa kuwa ni tabia ambayo watu wamekuwa nayo kwa muda mrefu na ni vigumu kuwaomba watu kubadili mawazo na mienendo yao,” alisema.

Kampuni hutoa zawadi za vocha za kununua mafuta au data ya mtandao kwa familia zinazohiari kushiriki vuguvugu la uundaji upya. Bw. Honu alisema kwamba wanawaambia watu, “Tupatieni taka zenu za plastiki nasi tuwape vocha za mafuta ya magari yenu.”

Bw. Honu aliongeza kuwa “watu wanaopokea mapato ya chini ya dola 5 kwa siku hutupatia taka zao za plastiki nasi huwapa pesa au data ya mtandao. Unalotakiwa kufanya ni kuhakikisha umewasilisha taka yako ya plastiki au uhakikishe tumeichukua kutoka kwako. Kisha unaamua unataka zawadi gani.”

Baadaye kampuni inawasilisha plastiki zilizokusanywa kwa kampuni ya kuunda upya.

Kulingana na Shirika la Kulinda Mazingira la Ghana, takriban tani milioni 2.58 za plastiki ghafi huagizwa nchini kila mwaka, na 73% yake hugeuka taka, lakini 19% hutumiwa tena. Ni chini ya 0.1% ya taka huundwa upya.

Huku akitambua kwamba ni sehemu ndogo mno ya taka za plastiki zinaundwa upya, Bw. Honu alisema: “Tunastahili kuanza kubadili mkondo kwa vyovyote vile.” Huenda ikachukua muda mrefu, ila anaendelea kuhamasishwa na ari yake kuhakikisha kwamba rafiki yake hakufariki bure.

Koliko Wear: huunda upya vitambaa vya mtumba kuwa viatu vya mtindo wa hadhi

Alikuwa akimsaidia rafiki yake kuipiga jeki biashara yake ya kutengeneza viatu kabla ya kujitosa katika mtindo wa kiikolojia kwa kuunda viatu kutokana na malighafi yaliyotumika.

“Kitaaluma mimi ni mhudumu wa benki, ila sasa mimi ni mtengeneza viatu. Ninatumia malighafi yaliyoundwa upya kutengeneza viatu,” Peter Kweku Anowie aliambia Africa Renewal

Biashara ya Anowie ya Koliko Wear huunda viatu kutokana na vitambaa vilivyotumika vya jinzi, pamba ya samani, shuka, magunia ya katani na mipira ya tairi za magari zilizotumika.

Kwake mpito kutoka kwa huduma za benki hadi kwa ujasiriamali ulifanyika kibahati. Alisema, “Ninatoka Takoradi, magharibi mwa Ghana. Siku moja nilipatana kisadfa na rafiki mtengeneza viatu ambaye biashara yake ilikuwa ikiporomoka. Nilimwambia kuwa ningemsaidia kwa kuwekeza mtaji mdogo katika biashara yake, ili aendelee kufanya biashara.”

Baadaye, alipogundua kuwa kutengeneza viatu kunaweza kuwa na faida, Bw. Anowie aliamua kujitosa ndani kikamilifu. “Niliona kuwa ilikuwa biashara nzuri na bunifu, na nikajiuzulu kutoka kazi yangu benkini ili kuingia kikamilifu katika biashara ya kutengeneza viatu. Mimi ni mwanafunzi wa taaluma ya usimamizi wa biashara na niliegemea sana huduma za fedha za benki, kwa hivyo nina maarifa fulani kuhusu biashara.”

Bw. Anowie alitaka kuanzisha kitu ambacho kingeweza kuwapa vijana mafundisho na “kuwaonyesha jinsi ya kujitegemea kifedha, namna ya kuendesha mambo ili kuimarisha hali ya maisha yao.”

Baada ya miaka mitatu, biashara hiyo sasa imewaajiri takriban watu kumi na wawili. “Nina furaha kuu kwa kuwa ninaona kwamba watu wengine karibu nami wanapata mafundisho ya kutengeneza viatu. Mbali na kujipatia pesa, wanaweza kutunza marafiki na famila zao pana.”

Kama biashara nyingine za kiikolojia nchini Ghana, watu wanaojihusisha na KolikoWear wanalenga kukua na kuwa na athari kwa jamii. Kituo cha Ghana Climate Change Innovation Centre (GCCIC) kinasaidia, kutoa mafundisho na misaada mingine ya kiufundi.

“Nilijiunga na GCCIC mwaka jana tu, na ndio, wamenisaidia kuhakikisha kuwa rekodi zangu ziko sawa ili kuvutia wawekezaji,” alisema Bw. Anowie.